Tuesday, February 11, 2014

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA UCHUMI (SERA), MWINGULU LAMECK NCHEMBA, AMEKIMBILIA KWA MCHUNGAJI MAARUFU DUNIANI, TB JOSHUA NCHINI NIGERIA.



NAIBU Waziri wa Fedha na Uchumi (Sera), Mwingulu Lameck Nchemba, amekimbilia kwa Mchungaji maarufu duniani, TB Joshua, wa nchini Nigeria, kufanya toba, kuombewa na kupata kile kinachoaminika kuwa ni utakaso.


Mwingulu ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Magharibi (CCM), anaongeza idadi ya wanasiasa nchini wanaokimbilia kwa TB Joshua kuombewa, kufanya toba na kupata utakaso unaoaminika kwamba unaweza kuwasaidia katika harakati zao za kisiasa.


Mmoja wa wanasiasa waliopata kufika kwa mchungaji huyo nchini Nigeria na kuibua mjadala nchini ni pamoja na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, Mbunge wa Monduli (CCM).


Akiwa kanisani hapo juzi, huku akionekana moja kwa moja na Kituo cha Televisheni cha Emmanuel, Mwigulu akiwa amevalia skafu shingoni kama kawaida yake, aliinuliwa na TB Joshua na kujitambulisha kwa majina yake matatu kwamba anaitwa Mwigulu Lameck Nchemba.


Kabla ya kumuinua Mwigulu, Nabii Joshua alikuwa akizungumzia namna ya kumuita Yesu Kristo. Aliwaambia waumini wake waliofurika katika kanisa hilo maarufu duniani kuwa jina la Yesu linaitwa mara moja na anasikia na kutenda kazi mara moja, lakini ukiona unamwita Yesu mara nyingi bila kukuitikia, ujue huyo si Yesu Kristo Mnazareth.


Wakati akisema maneno hayo, Mchungaji Joshua alisogea hadi mahala alipokuwa ameketi Mwigulu na waumini wengine na kumtaka asimame, huku akiwaomba waumini waangalie mfano aliokuwa akiutoa kwa Naibu Waziri huyo wa Fedha.


Mazungumzo kati ya Mwingulu na Mchungaji Joshua yalikuwa hivi:


TB Joshua: Wewe Bwana unaitwa nani


Mwigulu: Naitwa Mwingulu


TB Joshua: Taja majina yako matatu


Mwingulu: Naitwa Mwigulu Lameck Nchemba


Baada ya utambulisho huo, TB Joshua alijaribu kuyaita majina yote matatu ya Mwigulu, lakini alishindwa kwa kutamka vibaya na baadaye akamtaka Mwigulu amwite Mchungaji Joshua kwa jina lake.


Kabla ya Mwigulu hajaanza kumwita, Mchungaji Joshua alisogea hatua takriban kumi mbele ya Mwigulu, akiwa amempa mgongo Mwigulu na kumtaka amuite kwa jina lake.


Mwigulu alianza kumuita TB Joshua zaidi ya mara saba, lakini Naibu Waziri huyo hakugeuka nyuma wala kuitikia na ndipo alipowarejea waumini wake kwa kusema ukiona unaita jina la Yesu mara nyingi bila kuitikiwa, ujue unayemuita si Yesu.


Katika ibada hiyo, TB Joshua pia alisema Tanzania, Nigeria na nchi nyingine zinazokabiliwa na uchaguzi mkuu hivi karibuni zitakumbwa na matatizo makubwa ya hekaheka za uchaguzi, lakini aliwaonya viongozi watakaohusika na uvunjifu wa amani, hawataachwa salama na mkono wa Mungu.


Tanzania Daima..

Like · · Share · 5 hours ago ·

Tags:

0 Responses to “NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA UCHUMI (SERA), MWINGULU LAMECK NCHEMBA, AMEKIMBILIA KWA MCHUNGAJI MAARUFU DUNIANI, TB JOSHUA NCHINI NIGERIA.”

Post a Comment

Ila tafadhali sana angalia usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu.

HHHHHHHHHHHH

Subscribe

Kwa habari na Taarifa weka Email yako Hapa tutakutumia

© 2014 FUNUNU HABARI.. All rights reserved.
Designed by FUNUNU HABARI