Friday, June 28, 2013
Yanga yambania Kaseja, yamtwaa Dida wa Azam
Friday, June 28, 2013 by Unknown
MABINGWA wa soka Tanzania Bara, Yanga wamemtosa kipa na nahodha wa Simba, Juma Kaseja na badala yake kuamua kumsajili aliyekuwa kipa wa Azam FC, Deogratius Munishi ‘Dida.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Yanga, Abdallah Bin Kleb, Dida amesajiliwa baada ya ushauri wa Kocha Mkuu, Ernie Brandts na kipa namba moja wa mabingwa hao, Ally Mustafa.
Katika mahojiano na blogu ya BIN ZUBEIRY jana, Bin Kleb alikiri kuwa Kaseja alikuwa miongoni mwa mapendekezo ya majina ya kusajiliwa na mabingwa hao, lakini akazidiwa na Dida.
“Lakini kabla ya kumsainisha, tuliomba maoni ya watu mbalimbali akiwemo kipa wetu namba moja wa sasa, naye akatoa baraka zake kwamba Dida ndiye anayefaa,” alisema Bin Kleb katika mahojiano hayo.
Alisema kulikuwa kuna baadhi ya maoni yakipendekeza Kaseja aliyetemwa Simba baada ya kumalizika kwa mkataba wake, asajiliwe Yanga SC, lakini baada ya uongozi kujadili, ukaona ni bora kufuata mapendekezo ya kocha huyo Mholanzi kwa kumsajili Dida.
“Kulikuwa kuna majina ya makipa watatu, kati yao, wawili wote wamekwishawahi kudakia Yanga, Kaseja na Benjamin Haule, lakini katika majumuisho, Dida akawa ameshinda mchakato nasi tukamsainisha mkataba wa miaka miwili jana (juzi) mchana,” alisema Mwenyekiti huyo.
Alisema Dida aliyewahi pia kuidakia Mtibwa Sugar ya Manungu, Turiani, anachukua nafasi ya Said Mohamed aliyeachwa baada ya kumaliza mkataba wa miaka miwili. Alisajiliwa kutoka Majimaji ya Songea.
“Dida ni kipa mzuri, ana uzoefu wa kutosha. Ni kipa ambaye amekuwa akikubalika mbele ya makocha wengi wa timu ya taifa hapa nchini, tumeona atatufaa na tumempa mkataba wa miaka miwili,” alisema.
Kipa huyo sasa atakuwa mbadala wa Mustafa ‘Barthez,’ aliyewahi kudaka pamoja wakiwa katika klabu ya Msimbazi. Yanga inaye kipa mwingine, Yaw Berko, ingawa siku zake Jangwani zinahesabika.
Kaseja alitangazwa kutoongezewa mkataba wake mapema wiki hii na Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage, na tangu hapo taarifa zimekuwa zikimhusisha na kuhamia Yanga, Azam na Coastal Union ya Tanga.

This post was written by: Author Name
Author description goes here. Author description goes here. Follow him on Twitter
Get Updates
Subscribe to our e-mail newsletter to receive updates.
Related Articles
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 Responses to “Yanga yambania Kaseja, yamtwaa Dida wa Azam”
Post a Comment
Ila tafadhali sana angalia usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu.