Sunday, April 7, 2013

Tomas Rosicky azinogesha hesabu za Wenger za nafasi ya pili.



Baadhi ya mashabiki wa soka ambao awali hawakuzielewa uzuri hesabu za Arsene Wenger za kwamba timu yake sio tu kwamba itashiriki Ligi ya mabingwa Ulaya msimu ujao, bali pia inaweza kumaliza ikiwa nafasi ya pili, wanatakiwa kuuangalia vyema msimamo wa ligi kuu ya Uingereza hivi sasa.

Jioni ya leo, vijana wa kocha huyo mfaransa, wameendelea kuziwekea vinogesho hesabu za kocha wao baada ya kuonyesha kandanda safi na kufanikiwa kuibuka na pointi tatu muhimu dhidi ya West Brom Alibion, katika mechi ambayo Arsenal walimaliza wakiwa pungufu.

Tomas Rosicky aliyarejea makali yake ya enzi hizo, kwa kutupia nyavuni bao mbili peke yake, moja katika kila kipindi, na kuwahakikishia Arsenal pointi tatu ambazo sasa zinawafanya kukaa katika nafasi ya nne, iliyo ya mwisho kwa timu zinazocheza ligi ya mabingwa.

Ushindi huo umewawezesha kufikisha pointi 56, ikiwa ni pointi sita tu nyuma ya Man City wanaoshika nafasi ya pili na pointi moja nyuma ya Tottenham Hotspurs wanaoshikilia nafasi ya tatu na pointi moja juu ya Chelsea ambao wanashuka dimbani kesho jioni.

Katika mechi hiyo, nyota njema kwa Rosicky, ilianza kuonekana mapema baada ya kufanikiwa kuokoa shuti la Claudio Yacob katika mstari wa lango lao na kisha kuwanyanyua mashabiki kwa shangwe baada ya kufunga bao maridadi kwa kichwa cha karibu na lango akiunganisha krosi ya Gervinho.

Kiungo huyo wa kimataifa wa Jamhuri ya Czech, alihitimisha siku njema kwake kwa kufunga bao la pili katika kipindi cha pili ambapo aliusukumia nyavuni mpira uliokuwa umetemwa na kipa wa West Brom.

Kabla ya kufunga bao hilo, Rosicky alikuwa amepokea pasi toka upande wa kulia ikiwa imetoka kwa Aron Ramsey, ambapo aliudhibiti mpira huo na kuachia shuti kali lililotemwa na kipa Ben Foster na kasiya kipa huyo kutaka kuurejea mpira huo ilizidiwa na ile ya Rosicky ambaye aliuwahi na kuutumbukiza kimiani.

Arsenal hata hivyo walimaliza pambano hilo wakiwa pungufu baada ya beki wao wa kati Per Mertesacker kulimwa kadi nyekundu dakika ya 70 baada ya kumchezea rafu Shane Long aliyekuwa katika nafasi ya kufunga. Adhabu hiyo pia ilipelekea West Brom kuzawadiwa penalti iliyowekwa kimiani na James Morrison.

Upungufu huo wa Arsenal uliwapa wenyeji Albion nguvu ambapo kwa dakika zilizosalia walisukuma mashambulizi na kuweka kambi nusu ya upande wa Arsenal, lakini vijana hao wa Wenger walikomaa na kuhakikisha wanamaliza dakika 90 wakiwa washindi.

Katika mechi zingine zilizopigwa jioni ya leo, Reading waliokuwa nyumbani waliangukia pua baada ya kukubali kipigo cha bao 2-0 dhidi ya Southampton, huku Swansea wakitoka sare ya 2-2 dhidi ya Norwich. Stoke nao walikubali kipigo cha bao 3-1 dhidi ya waliokuwa wageni wao Aston Villa.

Msimamo wa ligi baada ya mechi za leo ni kama unavyoonekana hapa chini:


Tags: ,

0 Responses to “Tomas Rosicky azinogesha hesabu za Wenger za nafasi ya pili.”

Post a Comment

Ila tafadhali sana angalia usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu.

HHHHHHHHHHHH

Subscribe

Kwa habari na Taarifa weka Email yako Hapa tutakutumia

© 2014 FUNUNU HABARI.. All rights reserved.
Designed by FUNUNU HABARI